RC CHALAMILA AWEKA MIKAKATI KUKABILIANA NA HADHARI ZA MVUA
habariNa Dotto
Mwaibale, Dar es Salaam
MKUU wa Mkoa
wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amesema jiji hilo limejipanga kuchukua
tahadhari zote zitakazotokana na hadhari za mvua za masika ambazo zinaendelea
kunyesha.
Chalamila
aliyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam
Aprili 18, 2025 wakati akitoa taarifa kwa wananchi kuhusu kuchukua tahadhari
katika kipindi hiki cha msimu wa mvua za masika zilizoanza kunyesha mwezi Machi hadi mwezi Mei
2025 na mikakati iliyopo ya kukabiliana na hadhari hizo.
Mkuu huyo wa
mkoa alisema hatua ya kwanza iliochukuliwa ni kufanya malipo ya fidia mbalimbali kwa
watu wote waishio mabondeni na kuanza kwa utekelezaji wa ujenzi wa barabara ya
juu kuanzia eneo la Fire hadi Magomeni na kulipa fidia kwa wakazi wa bonde la
Mto Msimbazi kwa ajili a mradi wa kuendeleza bonde hilo ili kukabiliana na
mafuriko sanjari na kuboresha matumizi ya ardhi katika eneo hilo.
Aidha,
Chalamila alitoa maelekezo kwa idara za ujenzi na uokoaji kuhakikisha
wanajipanga kwenye kuimarisha miundombinu korofi na kuwa tayari kwa kuzuia na
kufanya uokozi wa haraka pale majanga yatakapojitokeza.
“Mpaka sasa kwa mradi wa kuendeleza bonde la Mto Msimbazi gharama za mradi huo ni takribani Dola za Marekani Milioni 260 ambapo Benki ya Dunia imetoa mkopo wa Dola za Marekani Milioni 200, Serikali ya Hispania imetoa mkopo wa Dola za Marekani Milioni 30 na Serikali ya Uholanzi imetoa ruzuku ya Euro Milioni 30,” alisema Chalamila na kueleza kuwa miradi hiyo itaanza kutekelezwa wakati wowote kuanzia sasa.
Kutokana
na tahadhari hiyo amezitaka taasisi za Serikali mkoani hapa kuwa tayari
kukabiliana na changamoto mbalimbali ambazo zitaletwa na mvua hizo.
“Mkoa wetu
umejipanga vizuri kukabiliana na changamoto hizo iwapo zitajitokeza,". alisema Chalamila.
Wakati huo
huo akizungumzia kuhusu hali ya usalama kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi oktoba mwaka huu, Chalamila amewaondoa hofu na kuwahakikishia usalama wafanyabiashara katika jiji hilo wa
kutoka nje na ndani ya nchi.
Aidha, amepongeza mafanikio makubwa yanayoendelea kupatikana
baada ya maboresho makubwa ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) chini ya Kampuni ya DP
Word ya Dubai.
Alisema wanasiasa wengi wanakiri Serikali imefanya kazi
kubwa ya ujenzi wa miradi mbalimbali kupitia makusanyo ya ndani ambapo
aliwahimiza wananchi kuendelea kulipa kodi ili miradi mingine ya kimkakati
ifanyiwe kazi ipasavyo.
"Kwa sasa tupo katika kipindi cha kuelekea kwenye
Uchaguzi Mkuu, hivyo inawezekana baadhi ya wafanyabiashara wakawa na hofu,
ninachoweza kuwaambia wasiwe na hofu kwani sisi kama mkoa tumejipanga
kuhakikisha utulivu na amani inaendelea wakati wa uchaguzi na baada uchaguzi,”
alisema Chalamila.
Katika tukio
jingine kwenye mkutano huo, Chalamila amewaomba wadau mbalimbali kujitoa
kuwasaidia Wasanii wafupi wakiongozwa na Tausi Degela, Pimbi na Hamisi, ili kuwapatia gari jipya wasanii hao kwa ajili ya
shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya miradi
mbalimbali inayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan na kumuombea
kura wakati kampeni za uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi okoba mwaka huu.
“Watu wenye ulemavu, wakiwemo wasanii wafupi, ni sehemu muhimu ya jamii na wanayo nafasi ya kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa letu na kutoa elimu sahihi kuhusu mafanikio ya Serikali,” alisema Chalamila.
Msanii
Tausi Mdegela aliwataka watu wenye ulemavu kuachana na dhana ya utegemezi na
kuanza kujishughulisha na shughuli za uzalishaji mali, akisisitiza kuwa ulemavu
si kikwazo cha mafanikio.
“Tumewezeshwa
kupitia mikopo na fursa nyingine. Tunapaswa kujiamini na kushiriki kikamilifu
katika kuinua uchumi wetu binafsi na wa jamii,” alisema Tausi.
Naye,
msanii Pimbi akizungumza baada ya kupatiwa nafasi na mkuu wa mkoa alitumia
nafasi hio kuhamasisha watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika mchakato
wa uchaguzi mkuu huku akisisitiza kuwa ushiriki wao ni wa muhimu katika maamuzi
ya kitaifa.
“Ni wakati wetu wa kusimama na kuonekana. Tuna haki sawa kama Watanzania wengine, na tunapaswa kutumia sauti yetu ipasavyo,” alisema Pimbi.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, akiwa na Wananii wa kundi la Wajuu wa Mama.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, akisisitiza jambo kwenye mkutano huo na waandishi wa habari.
HISTORIA YAANDIKWA :BILIONI 4.6 KUENDELEZA BUNIFU ZA WATANZANIA
habariKatika hatua ya kihistoria ya kuwezesha mapinduzi ya kiuchumi kupitia teknolojia na ubunifu wa vijana, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo imezindua rasmi mpango wa uwezeshaji kwa wabunifu wa Kitanzania wenye thamani ya shilingi bilioni 4.6.
Mpango huo unatekelezwa kupitia ushirikiano kati ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) na CRDB Foundation, ukiwa na lengo la kugeuza mawazo ya wabunifu kuwa miradi hai ya biashara na viwanda.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, akizindua mpango huo, alisema kuwa kati ya hizo bilioni 4.6, Serikali kupitia COSTECH imetoa dhamana ya shilingi bilioni 2.3, huku CRDB Foundation ikitoa kiasi kilichosalia kama mikopo nafuu kwa wabunifu waliokidhi vigezo.
“Hili ni jambo la kipekee. Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameelekeza wazi kuwa vijana wabunifu wawezeshwe, na leo tumeona matokeo ya dhamira hiyo. Serikali haikubaki nyuma, imetoa dhamana ya bilioni 2.3 ili kuhakikisha hakuna mkwamo wa kifedha kwa wabunifu wetu,” alisema Prof. Mkenda.
Ameongeza kuwa Tanzania haiwezi kufikia maendeleo ya kweli bila kutoa kipaumbele kwa ubunifu, hasa kwa vijana, ambao ndio nguvu kazi ya taifa.
Alisisitiza kuwa serikali iko tayari kushirikiana na taasisi za umma na binafsi katika kuhakikisha kuwa kila wazo lenye tija linapata msukumo wa kifedha, kitaalamu na kiutendaji.
Katika hafla hiyo, Prof. Mkenda aliwapongeza CRDB Foundation kwa ujasiri wao wa kuwekeza kwa wabunifu wa Kitanzania, akisema huo ni mfano wa taasisi binafsi zinavyoweza kuchangia maendeleo ya kitaifa. “Taasisi nyingine zijifunze kutoka CRDB Foundation.
Vijana wetu hawahitaji huruma, wanahitaji fursa. Na tukiwapa fursa, watafanya maajabu,” alisema huku akiwasihi wadau wengine kujitokeza kuwekeza kwa wabunifu wa ndani.
Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alieleza kuwa zaidi ya wabunifu 400 kutoka mikoa mbalimbali nchini tayari wamenufaika na programu za uwezeshaji za COSTECH, na wengi wao wapo katika hatua ya kupokea mikopo.
Alibainisha kuwa mikakati kama hii ni utekelezaji wa moja kwa moja wa ahadi za Rais Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha vijana na kutumia maarifa, sayansi, teknolojia, na ubunifu kama suluhisho la changamoto za maendeleo.
Miongoni mwa maeneo yanayopatiwa kipaumbele ni pamoja na teknolojia za kidijitali, akili-bandia (AI), na suluhisho bunifu kwa changamoto za kijamii kama afya, kilimo, na elimu.
Profesa Mkenda alisisitiza umuhimu wa kuingiza masomo ya akili-undi kwenye mitaala ya elimu ili kuandaa kizazi chenye uwezo wa kukabiliana na ushindani wa soko la kimataifa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Foundation, Bi. Tully Esther Mwambapa, alisema kuwa taasisi hiyo imeamua kushirikiana na COSTECH kama njia ya kuendeleza miradi yenye mwelekeo wa biashara na athari kwa jamii.
“Tunatambua kuwa ubunifu ni injini ya maendeleo. Kupitia uwekezaji huu, tunawaleta vijana karibu na fedha, maarifa, na mitandao ya ukuaji. Lengo letu ni kusaidia kubadilisha maisha yao na jamii kwa ujumla,” alisema Bi. Mwambapa.
Kwa ujumla, uzinduzi huu unafungua ukurasa mpya wa maendeleo ya ubunifu nchini. Historia imeandikwa—wakati umefika kwa wabunifu wa Kitanzania kuinuka, kushirikiana na wadau, na kuwa sehemu muhimu ya ujenzi wa uchumi wa viwanda na maarifa.
Kupitia uwekezaji huu wa bilioni 4.6, Tanzania sasa inatengeneza mazingira wezeshi kwa vijana kuandika kesho yao kupitia maarifa, teknolojia na uthubutu.







