VIJANA 1376 IFAKARA WANUFAIKA NA MRADI WA YEE

April 01, 2017
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Jumla ya vijana 1376 wa Wilaya ya Ifakara mkoani Morogoro wamenufaika na mradi wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi (YEE) unaofadhiliwa na Jumuiya ya Ulaya (EU) na kuratibiwa na Shirika lisilokuwa la Kiserikali la Plan International.
Takwimu hizo zimetolewa leo mkoani humo na Meneja wa Shirika hilo Wilaya ya Ifakara, Majani Rwambali alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya maendeleo ya mradi huo unaotarajia  kuisha mwaka 2018.
Rwambali amesema mradi huo umeanza tangu mwaka 2015,  unatekelezwa katika Mikoa mitano ikiwemo ya Dar es Salaam, Lindi, Mtwara, Pwani na Morogoro ambapo vijana wanaoishi katika mazingira magumu wanapewa elimu ya mafunzo ya ufundi katika fani mbalimbali ili waweze kujitegemea na kujikwamua kimaisha.
“Kwa wilaya yetu mradi huu unatekelezwa katika Kata 9 zikiwemo za Mwaya, Mkula, Mchombe, Kibaoni, Mgeta, Kiberege, Ifakara, Lumemo na Mbongo ambapo hadi sasa jumla ya vijana 1376 kati ya vijana 1490 waliokuwa kwenye lengo la mradi wameshapatiwa mafunzo na wengi wao wameshajiajiri”alisema Rwambali.
Meneja amefafanua kuwa mafunzo hayo hufanyika kwa awamu ambako mpaka sasa awamu zilizofanyika ni nne huku ikibaki awamu moja itakayohusisha vijana waliosalia kukamilisha lengo la mradi huo ambao inategemewa kuanza miezi michache ijayo kwani.
Aidha, Rwambali ameongeza kuwa mradi huo umekua na changamoto katika kuwapata vijana wenye ulemavu kwa sababu jamii bado haijatambua kuwa vijana hao wana uwezo wa kufanya kazi na kujipatia vipato sawa na vijana wengine hivyo ametoa rai kwa vijana hao kujitokeza kwa wingi katika awamu hiyo ya mwisho ya mradi huo.
Kwa upande wake Katibu wa watu wenye ulemavu wa ngozi wilayani Kilombero, Hamis Liundi ameishukuru Umoja wa Ulaya kwa kuwaletea mradi huo uliowafikia hadi vijana wenye ulemavu na kuboresha maisha yao  ingawa bado kuna changamoto za vifaa vya kufanyia kazi pamoja na maeneo kwa ajili ya ofisi.
“Mradi huu ulianza wakati wa kampeni hivyo watu hawakuufatilia kutokana na kuhusisha mradi huo na mambo ya kisiasa, uchaguzi umeshapita hivyo ninawaomba vijana wenzangu hasa walemavu kujitokeza kwani fursa kama hizi zinatokea mara chache,” alisema Liundi.
Nae mmoja wa walemavu wa viungo aliyenufaika na mradi huo, Elia Limota amesema kuwa mradi huo umemuwezesha kutambulika katika jamii na kumfanya awe kijana anayeweza kujitegemea kwani baada ya mafunzo hayo yeye pamoja na walemavu wenzie wameweza kuunda kundi na kuvumbua miradi mbalimbali ikiwemo ya uchomaji wa matofali, ukodishaji wa baiskeli pamoja na kilimo cha mpunga.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »