
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI
📌 Matumizi ya teknolojia kupewa kipaumbele Sekta ya Nishati
📌 Morocco wampongeza Rais Samia kwa usimamizi bora Sekta ya Nishati
Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati
Tanzania na Ufalme wa Morocco zimekubaliana kuimarisha ushirikiano wa matumizi ya teknolojia katika Sekta ya Nishati ili kuiwezesha sekta hiyo kuwa na mchango endelevu nchini.
Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko alipokutana na Mwenyeji wake Waziri wa Mageuzi ya Nishati na Maendeleo Endelevu wa Ufalme wa Morocco, Mhe. Leila Benali kuzungumza kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya nishati ili kuimarisha ushirikiano na nchi ya Morocco.
"Mwaka 2016 Tanzania na Morocco zilisaini hati ya makubaliano (MoU) ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya umeme, mafuta na matumizi ya nishati mbadala ili yapewe kipaumbele katika nchi hizo, ". Amesema Dkt. Biteko
Mhe. Dkt. Biteko amesema pamoja na maendeleo ya nishati yaliyofikiwa, bado nchi inahitaji uwekezaji zaidi katika sekta ya nishati mbadala ikiwa na matarajio ya kukuza shughuli za kiuchumi hususan katika sekta za viwanda na madini jambo ambalo linahitaji uwekezaji wa kimkakati zaidi katika sekta ya nishati.
Ametaja mambo mengine ni pamoja na kubadilishana uzoefu miongoni mwa wataalam katika sekta ya nishati ikilenga kuifanya kuwa na tija kwa taifa na uchumi kwa ujumla.
Kwa upande wake, Waziri wa Mageuzi ya Nishati na Maendeleo Endelevu wa Ufalme wa Morocco, Mhe. Leila Benali amesema kuwa Tanzania inaweza kubadilisha sura yake kwa kuwa na juhudi za pamoja za kuunganisha rasilimali zilizopo kuhakikisha nishati ya umeme inawafikia wananchi wengi zaidi.
Amesema hakuna maendeleo yanayoweza kupatikana gizani hivyo, njia ya kuleta maendeleo na ustawi wa watu ni kuwaangaza maisha yao kwa kupitia sekta ya Nishati.
Aidha, Mhe. Benali amepongeza kwa dhati juhudi za Rais Samia kuwa kinara wa maendeleo ya nishati safi ya kupikia, Tanzania na Afrika kwa ujumla.
Katika ziara hiyo, Dkt. Biteko ameongozana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Mhe. Dennis Londo, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi katika eneno la Morocco, Mhe. Ally Mwadini, Wataalam mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati, Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC).
Mwisho.
*📌 Maeneo 300 tayari yamefikkwa*
*📌 Asisitiza gharama ya kuunganisha umeme Vijijini ni shilingi 27,000/-*
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe Judith Kapinga amesema Serikali inaendelea kutekeleza mradi wa kupeleka umeme kwenye maeneo ya kimkakati nchini ikiwemo maeneo ya migodi midogo, maeneo ya uvuvi, Viwanda na yanayochagiza shughuli za kiuchumi.
Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Mei 14, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la la Mbunge wa Mwibara, Mhe. Charles Kaijage aliyetaka kufahamu mkakati wa Serikali kuyapelekea umeme maeneo ya uvuvi ili kukuza uchumi wa wananchi wa maeneo hayo.
"Mheshimiwa Naibu Spika Mradi huu wa kupeleka umeme maeneo ya kimkakati umefikia zaidi ya maeneo 300 ikiwemo vituo vya afya na visima vya maji kwa maeneo ambayo yanatoa huduma za kijamii." Amesema Kapinga
Akijibu swali la Mbunge wa Igunga, Mhe. Nicholas Ngassa aliyeuliza lini Serikali itaanza usambazaji umeme kwenye Vitongoji vya Jimbo la Igunga. Mhe. Kapinga amesema Jimbo la Igunga lina jumla ya Vitongoji 337 ambapo kati ya hivyo, Vitongoji 95 vimepatiwa umeme.
Ameongeza kuwa, katika Vitongoji 15 Wakandarasi wanaendelea na utekelezaji wa miradi kupitia Mradi wa Kupeleka Umeme Vitongojini Awamu ya Pili A (HEP IIA) na Vitongoji 69 zabuni imetangazwa kupitia Mradi wa Kupeleka Umeme Vitongojini Awamu ya Pili B (HEP IIB).
Amesema kuwa, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) itaendelea kutenga fedha za kuvipelekea umeme vitongoji 158 vilivyosalia.
Amesisitiza kuwa, gharama ya kuunganisha umeme kwa maeneo ya Vijijini ni shilingi 27,000/- na kuongeza kuwa, kuna mradi utakaoanza hivi karibuni unaohusisha Vitongoji ambavyo havina laini kubwa ya umeme na vilivyo na kwenye laini kubwa ya umeme.