Showing posts with label habari. Show all posts
Showing posts with label habari. Show all posts

Wafanyabiashara Wapongeza TRA kwa Uelewa wa Sheria Mpya za Kodi

August 17, 2025 Add Comment
Na mwandishi wetu, Simiyu

Wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu wameiomba Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutoa elimu ya kodi mara kwa mara ili kila mwananchi afahamu umuhimu wa kulipa kodi kwa maendeleo ya Taifa.

Wakizungumza wakati wa semina ya mabadiliko ya sheria za kodi kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya TRA mkoani Simuyu, wafanyabiashara hao wamesema kuwa, elimu ya kodi ikitolewa kila mara, itasaidia watu kujua faida za kodi na hivyo kupunguza vitendo vya ukwepaji kodi.

“Tunaomba elimu hii iendelee kutolewa mara kwa mara, yapo makundi mengi leo hii hayajapata elimu hii, tunawaomba TRA iwafikie na wao, hii itapunguza kwa kiwango kikubwa watu kukwepa kodi na kujua umuhimu wa kulipa kodi,” alisema Bw. Elias Nungwana.

Bw. Mbowe Malemi ambaye ni mfanyabiashara wa Bariadi mjini mkoani humo, ameishukuru TRA kwa kuwapa elimu ya mabadiliko ya sheria hizo, na kueleza kuwa, sheria mpya nyingi ambazo zimebadilishwa ni rafiki kwao na zitawasaidia katika kuongeza mwamko wa kulipa kodi.

“Tunawashukuru sana TRA kwa huu utaratibu, kila mwaka tumeanza kuona wanakuja kutupa elimu jambo hili linatufanya tulipe kodi kwa hiari kwani tunakuwa na uelewa wa sheria mpya na zile za zamani,” alisema Bw. Malemi.

Kwa upande wake Meneja Msaidizi wa TRA Mkoa wa Simiyu Bw. Honest Mushi alisema kwamba, kutolewa kwa elimu hiyo kwa walipakodi mkoani humo, itasaidia Mamlaka hiyo kufikia lengo la mkoa ambalo ni shilingi bilioni 30.4 katika mwaka huu wa fedha 2025/2026.

Meneja Msaidizi huyo alisema kuwa, walipakodi katika mkoa huo wamekuwa wakitoa ushirikiano mkubwa kwa Mamlaka hiyo, hali ambayo imewezesha kuvuka lengo kwa kukusanya zaidi ya asilimia 100 katika mwaka wa fedha uliopita wa 2024/2025.

Naye, Afisa Msimamizi Mkuu wa Kodi kutoka TRA Bi. Eugenia Mkumbo alisema lengo la elimu hiyo ni kuwawezesha walipakodi kutambua na kuelewa wajibu wao katika suala zima la ulipaji kodi kwa hiari.

“Tunawaomba walipakodi wote kuhakikisha wanatimiza wajibu wao kama inavyoelekezwa kwenye sheria za kodi, baada ya elimu hii kila mmoja awe ametambua wajibu wake na kwa muda gani anatakiwa kulipa kodi,” alisema Bi. Eugenia.

Timu ya maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania inapita katika maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kutoa elimu ya mabadiliko ya sheria za kodi yaliyotokea mara baada ya kupitishwa kwa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Meneja Msaidizi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Simiyu Bw. Honest Mushi akifungua semina ya wafanyabiashara kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/2026 iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya TRA mkoani humo.
Afisa Msimamizi Mkuu wa Kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bi. Eugenia Mkumbo akiwasilisha mada ya mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/26 katika semina ya wafanyabiashara iliyofanyika iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya TRA mkoani Simiyu.
Baadhi ya Walipakodi waliohudhuria semina ya mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/26 wakifuatilia kwa makini semina hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya TRA mkoani Simiyu.
Baadhi ya Walipakodi waliohudhuria semina ya mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/26 wakifuatilia kwa makini semina hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya TRA mkoani Simiyu
.
Mshauri wa Kodi kutoka Kampuni ya Finx Capital House Bw. Jackson Samwel akitoa maoni yake wakati wa semina ya wafanyabiashara kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/2026 iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya TRA mkoani Simiyu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bariadi Education Centre Limited Bi. Elizabeth Yuma akichangia hoja wakati wa semina ya wafanyabiashara kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/2026 iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya TRA mkoani Simiyu.Mfanyabiashara wa Vifaa vya Ujenzi Bw. Enock Ntaniko akichangia hoja wakati wa semina ya wafanyabiashara kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2025/2026 iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya TRA mkoani Simiyu.

TPDC Runners Club yashiriki kwa kishindo CRDB Marathon 2025

August 17, 2025 Add Comment

Dar es Salaam, Agosti 17, 2025 – TPDC Runners Club leo imeungana na maelfu ya wakimbiaji kushiriki mbio kubwa za CRDB Marathon zilizofanyika katika Viwanja vya Farasi, Masaki, jijini Dar es Salaam. Mbio hizo zimehusisha umbali wa KM 5, KM 10, KM 21 na KM 42 na kuvutia washiriki kutoka taasisi mbalimbali za kiserikali, sekta binafsi na wananchi kwa ujumla.

REA YAHAMASISHA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KWA WAJASIRIAMALI SONGWE

August 16, 2025 Add Comment
-Wahamasishwa kuchangamkia fursa zilizopo kwenye eneo hilo

TANZANIA,BURUNDI ZAZINDUA UJENZI WA RELI YA SGR UVINZA- MUSONGATI

August 16, 2025 Add Comment




*_Kugharimu dola za Marekani bilioni 2.154_*


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa leo (Jumamosi, Agosti 16, 2025) ameshiriki uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa reli ya kisasa ya kutoka Uvinza hadi Musongati na kuwahahikishia Watanzania na WanaBurundi kwamba ujenzi huo utaanza katika muda uliopangwa.


Waziri Mkuu ambaye ameshiriki hafla hiyo kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema reli hiyo itakayokuwa na urefu wa km.240 pindi  ikikamilika, itakuwa ndiyo reli ya kwanza inayounganisha nchi na nchi katika ukanda wa Afrika Mashariki. 

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika eneo la Musongati, Burundi,  Waziri Mkuu amesema kukamilika kwa ujenzi wa reli hiyo kutasaidia kuunganisha masoko na kuendeleza biashara baina ya Tanzania na Burundi. 


"Reli ikikamilika itafungua fursa kwa wananchi wetu ambao wataweza kutoka hapa hadi Dar es Salaam ndani ya siku moja. Hata kwenye usafirishaji wa mizigo, hivi sasa, lori linatumia saa 96 kutoka Dar hadi Bujumbura lakini baada ya kukamilisha ujenzi, usafirishaji wa mizigo kwa kutumia treni utatumia saa 20 tu."

"Mradi wa reli ya kisasa siyo tu kwamba utarahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo, bali pia utafungua milango ya fursa mpya za uwekezaji na biashara kati ya Tanzania na Burundi."


Akielezea kuhusu mradi huo, Waziri Mkuu amesema ujenzi wa reli hiyo utagharimu dola za Marekani bilioni 2.154 na unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitano na  kwamba mwaka mmoja baada ya ujenzi utakuwa ni wa matazamio. 

Kwa upande wake, Rais wa Burundi,  Meja Jenerali Evarist Ndayishimiye alisema kuanza kwa ujenzi wa reli hiyo kutatibu shauku ya muda mrefu ya nchi hiyo kuwa na usafiri wa reli. 


"Leo ni siku ya furaha sana kwetu. Tumepata jawabu la tangu enzi na enzi. Mwaka 1921, mradi huu ulianzishwa na Wabelgiji kisha wakaja Wajerumani lakini wakashindwa. Leo hii Tanzania na Burundi tumeweza," alisema.

Alisema nchi yake imebarikiwa kuwa madini mengi na kuna wakati aliitisha kikao cha wawekezaji kutoka nchi kadhaa. "Wengi walivutiwa na wakataka kuwekeza mara moja, lakini wakaniuliza, tukianza kuchimba madini ya Nickel, tutayasafirishaje?"


"Hiyo changamoto ilitufanya tubungue bongo zetu na kutafuta suluhisho.  Tunaishukuru sana Serikali ya Tanzania kwa kukubali kuungana nasi ili tuanze mradi huu muhimu. Tukitoka hapa, tunataka reli iunganishe hadi Kindu, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC). Na baada ya hapo, tunataka reli yetu ifike Afrika Magharibi kwenye ufukwe wa bahari ya Atlantiki kwani tunaamini njia hiyo itaharakisha kuleta maendeleo."


Rais Ndayishimiye alimpongeza Rais Dkt. Samia kwa kufikia hatua kubwa za maendeleo. "Ukirudi nyumbani mwambie Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan kwamba tunampongeza sana kwa kuleta maendeleo ya haraka nchini Tanzania."


"Nimekaa Tanzania kwa muda mrefu lakini kwa sasa nikija naweza kupotea. Magomeni napajua, Tabata na Vingunguti napajua, Mwenge napajua, na Kinondoni nilishakaa; lakini kwa sababu ya maendeleo yaliyopatikana, naweza kupotea. Tunamshukuru kwa uongozi wake imara,"

Rais huyo alizungumza kwa Kiswahili na kuamsha shangwe miongoni mwa wananchi waliohudhuria tukio hilo. 


Mapema, Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa alisema utekelezaji wa mradi huo unaenda sambamba na Ajenda 63 ya Umoja wa Afrika ambayo inataka bara la Afrika liunganishwe kwa mtandao wa reli ya kisasa. 


Alisema mbali na kuziunganisha nchi hizo mbili, kukamilika kwa ujenzi wa reli hiyo, kutarahisisha kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo. "Hivi sasa, kontena moja la futi 20 linasafirishwa kwa gharama ya dola za Marekani 3,800 lakini reli ikikamilika, gharama itashuka hadi dola za Marekani 2,000.


Alisema faida nyingine itakayopatikana baada ya mradi huo kukamilika ni kuwezesha kusafirisha mizigo mingi kwa wakati mmoja. "Hivi sasa, mzigo unaosafirishwa kwa lori moja ni tani 30, lakini reli ikianza kazi, tutaweza kusafirisha tani 3,000 kwa wakati mmoja," alisema Waziri Mbarawa.


(Mwisho)

Imetolewa na 

Ofisi ya Waziri Mkuu, 

Jumamosi, Agosti 16, 2025

WAANDISHI WA HABARI DODOMA WAPATIWA MAFUNZO YA USALAMA NA ULINZI

August 16, 2025 Add Comment


Baadhi ya waandishi wa habari kutoka Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dodoma (Dodoma Press Club) wamepatiwa mafunzo ya usalama wa kimwili, kidijitali na afya ya akili, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kujilinda binafsi katika mazingira ya kazi.

Mafunzo hayo yalifanyika Agosti 16, 2025, yakiongozwa na Mkufunzi wa Usalama na Ulinzi, Okuly Julius, ambaye pia ni mwandishi wa habari. Okuly alipata mafunzo hayo kupitia Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na kisha kupewa jukumu la kuwajengea uwezo waandishi wenzake katika mikoa.

Akizungumza kwenye mafunzo hayo, Okuly amesema waandishi wa habari wanapaswa kuwa makini na kuchukua tahadhari muda wote kwani usalama huanzia kwa mwandishi mwenyewe.


“Ni muhimu kuchukua tahadhari kubwa dhidi ya mashambulizi ya kimtandao kwa kuhakikisha viunganishi vinavyopokelewa vinathibitishwa kabla ya kubofya, kutumia nywila imara na kuweka uthibitishaji wa hatua mbili. Waandishi wanapaswa kuwa makini zaidi hasa kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba 2025, kipindi ambacho mara nyingi huambatana na vitisho, ukatili na hata kukamatwa kiholela,” alisema Okuly.

Ameongeza kuwa ni vyema waandishi kutoa taarifa kwa watu wa karibu au wenzao wanapokwenda kwenye kazi, ili kuepuka hatari zinazoweza kutokea endapo watapatwa na matatizo wakiwa peke yao.

Kwa upande wao, baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Bahati Msanjila (Crown Media), Saida Issa (Gazeti la Zanzibar Leo), Rhoda Simba (Channel Ten), Gideon Gregory (Jambo FM) na Joyce Kasiki (Gazeti la Majira), walisema yamewajengea uwezo mkubwa na sasa wanafahamu mbinu bora za kufanya kazi kwa usalama.


Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa “Empowering Journalists for Informed Community” (Kuwawezesha Waandishi wa Habari ili Jamii Iweze Kupata Taarifa Sahihi) unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na Shirika la Maendeleo la Uswisi (SDC). Mradi huu unatekelezwa kwa ushirikiano wa International Media Support (IMS), Union of Tanzania Press Clubs (UTPC) na JamiiAfrica.