WAZIRI MAKAMBA AZINDUA BODI YA MFUKO WA TAIFA WA DHAMANA YA HIFADHI YA MAZINGIRA

February 02, 2017
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akiongea katika uzinduzi wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa dhamana ya Hifadhi ya Mazingira. Bodi hiyo iko chini ya Uenyekiti wa Bw Ali A. Mafuruki. Uzinduzi huo umefanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akiwakaribisha wajumbe wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa dhamana ya Hifadhi ya Mazingira (hawapo pichani), kulia ni Bw. Ali Mufuruki Mwenyekiti wa Bodi.


Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Eng. Ngosi Mwihava (kushoto) akiwa na Bw. Ali Mufuruki Mwenyekiti wa Bodi, wakati wa halfa ya uzinduzi wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa dhamana ya Hifadhi ya Maizngira jiini Dar es Salaam.



Sehemu ya Wajumbe wa Bodi (mstari wa mbele) wakifuatilia maelezo ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba katika hafla ya uzinduzi wa Bodi na Mfuko wa Dhamana ya Mazingira.






Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa dhamana ya Hifadhi ya Mazingira, mara baada ya kuizindua hii leo, Mtaa wa Luthuli jijini Dar es Salaam.



Na Lulu Mussa
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Muungano na Mazingira Mh. January Makamba hii leo amezindua Bodi ya Mfuko wa Taifa wa dhamana ya Hifadhi ya Mazingira Nchini iliyo chini ya Mwenyekiti Ali Mufuruki.
Waziri Makamba amesema Uzinduzi wa Mfuko  na Bodi hiyo utasaidia  upatikanani wa fedha za usimamizi wa Mazingira Nchini. “Ni matarajio yangu tutafanya kazi pamoja kuhakikisha mfuko unakuwa na fedha ya kutosha na unafanya kazi ili kukidhi malengo yaliyodhamiriwa hususan uboreshaji wa mazingira nchini” Alisisitiza Waziri Makamba
Waziri Makamba amesema  uteuzi wao una maana kubwa na kuwataka wajumbe wa Bodi hiyo kufanya kazi kwa kujituma na kuhakikisha kuwa Hifadhi ya Mazingira inakuwa ni ajenga ya kitaifa.
Waziri Makamba amewafahamisha wajumbe kuwa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 Kifungu cha 213 imeanzisha Mfuko wa Taifa wa Dhamana ya Hifadhi ya Mazingira ili kuhakikisha kuwa kunakuwepo fedha za kutosha za kulinda na kusimamia hifadhi ya mazingira nchini.
Aidha, tangu kuanzishwa kwa Mfuko huu kisheria, kumekuwepo na maandalizi mbalimbali ya kuhakikisha kwamba mfuko unaanza kufanya kazi mapema iwezekanavyo. Baadhi ya maandalizi hayo ni: Kufanya utafiti kuhusu vyanzo vya fedha kwa ajili ya Mfuko; kuandaa mwongozo wa kusimamia fedha za Mfuko; kuandaa kanuni za uendeshaji Mfuko; na kuwasilisha Wizara ya Fedha na Mipango mapendekezo ya vyanzo vya mfuko ili kupata utaratibu muafaka kwa kupata fedha hizo kwa ajili ya Mfuko.
Waziri Makamba amefanunua kuwa Malengo ya Mfuko wa Taifa wa Dhamana ya Hifadhi ya Mazingira kama yalivyobainishwa kwenye Sheria ya Mazingira ni pamoja na: Kusaidia utafiti unaolenga kuboresha hifadhi ya mazingira; Kujenga uwezo wa taasisi mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Makamu wa Rais, NEMC na nyinginezo katika hifadhi ya mazingira; Kutoa tuzo zinazolenga uhamasishaji wa hifadhi ya mazingira; Kutoa majarida yanayohusu hifadhi ya mazingira.

Malengo mengine ni pamoja na kutoa ufadhili kwa ajili ya mafunzo yanayohusu shughuli za    mazingira; Kusaidia jamii kwa kutoa misaada kwa ajili ya kutekeleza prgramu za hifadhi ya  mazingira; na Kulipia gharama za mikutano ya Kamati ya Mazingira ya Ushauri ya Taifa (National Environmental Advisory Committee - NEAC) na Bodi ya Wadhamini wa Mfuko, Waziri Makamba alisisitiza.
Waziri Makamba amesema kuwa juhudi za Serikali katika hifadhi ya mazingira zitakuwa endelevu na kuhakikisha kuwa Bodi itakuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha hifadhi ya mazingira inasimamiwa na kuendeshwa kwa mujibu wa Sheria kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa Dhamana ya Hifadhi ya Mazingira Bw. Ali Mufuruki amemuhakikishia Mhe. Waziri Makamba kuwa yeye na wajumbe wa bodi yake wako tayari kufanya kazi hiyo kwa heshima kubwa na kuhakikisha kuwa hifadhi na usimamizi wa mazingira unakua endelevu.
Bodi hiyo inaongozwa na Bw Ali Mufuruki ambaye Mwenyekiti na Mkurugenzi wa Kampuni ya Infotech, Mwajuma Mbogoyo, Imelda Teikwa, Profesa Razak Bakari Lokina na Hatibu Senkoro. Wengine ni Alesia Mbuya, Baraka Juma Kalangahe, Dkt. Andrew Komba na Profesa Yunus Mgaya.



Share this

Related Posts

Previous
Next Post »